Iran yasisitiza kuendeleza mpango wake wa makombora
Wizara ya Mashauri ya Kigeni ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran imesisitiza juu ya azma ya taifa hili ya kuendeleza mpango wake wa makombora.
Taarifa ya Wizara ya Mashauri ya Kigeni ya Iran imeeleza kuwa, mpango wa makombora wa Iran utaendelea kwa nguvu zote na kwa mujibu wa mipango iliyoandaliwa na taifa hili.
Taarifa ya Wizara ya Mashauri ya Kigeni ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran imetolewa leo ikiwa ni radiamali kwa hatua ya serikali ya Marekani ya kuongeza majina ya shakhsia na mashirika ya Kiirani katika orodha yake ya vikwazo vya makombora hatua ambayo ni kinyume cha sheria.
Wizara ya Mashauri ya Kigeni ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran imelaani vikali hatua hiyo ya Marekani na kuitaja kuwa, isiyokubalika na yenye kukinzana wazi wazi na sheria za kimataifa.
Sambamba na Wizara ya Mashauri ya Kigeni ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran kusisitiza kwa mara nyingine juu ya haki ya wazi na ya kisheria ya taifa hili ya kuinua kiwango chake cha ulinzi imesisitiza pia kwamba, Tehran itaendelea na mpango wake wa makombora wenye lengo la kuhifadhi, na kulinda mamlaka ya kujitawala taifa hili, mpango ambao katu haukinzani na mikataba ya kimataifa wala kukiuka azimio nambari 2231.