Zarif: Vikwazo vya Marekani havitaiburuza mezani Iran
Waziri wa Mambo ya Nje wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran amesema vikwazo vya kidhalmu vya Marekani katu haviwezi kuilazimisha Tehran iende kwenye meza ya mazungumzo wala kuifanya isalimu amri mbele ya matakwa ya Washington.
Mohammad Javad Zarif ameyasema hayo katika mahojiano na gazeti la The Guardian la Uingereza na kufafanua kuwa, duru mpya ya vikwazo hivyo dhidi ya Iran sio tu haitakuwa na taathira yoyote kwa taifa la Iran, bali italifanya listawi zaidi.
Mwanadiplomasia huyo wa ngazi za juu amekumbusha kuwa Wakala wa Kimataifa wa Nishati ya Atomiki hadi sasa umeshatoa ripoti chungunzima zenye kuthibitisha kuwa shughuli za nyuklia za Iran zinafanyika kwa malengo ya amani na kuongeza kwamba, bila shaka mafuta ya Iran yanaendelea kupata soko licha ya vikwazo hivyo.
Hapo jana pia Rais Hassan Rouhani wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran alisema kuwa, taifa hili litabakia kuwa huru na lenye mamlaka yake na katu halitasalimu amri mbele ya Marekani.
Tarehe 8 Mei mwaka huu, Rais wa Marekani Donald Trump alitangaza kujitoa nchi yake kwenye makubaliano ya nyuklia ya JCPOA na kurejesha tena vikwazo vya nyuklia dhidi ya Iran.
Jamii ya kimataifa imekosoa vikali maamuzi hayo ya Trump ambapo Uingereza, Ufaransa, Russia, China, Ujerumani na Umoja wa Ulaya zimetangaza kufungamana na JCPOA.