Nov 09, 2019 04:45 UTC
  • Javad Larijani akosoa vikwazo vya kidhalimu vya Marekani dhidi ya Iran

Katibu wa Idara ya Haki za Binadamu katika Vyombo vya Mahakama vya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran amekosoa kuendelea vikwazo vya kidhalimu vya Marekani dhidi ya Iran.

Mohammad Javad Larijani ameyasema hayo Ijumaa katika hotuba yake mbele ya Kikao cha 44 Kuhusu Ripoti za Baraza la Haki za Binadamu la Umoja wa Mataifa mjini Geneva na kuongeza kuwa: "Vikwazo vya Marekani dhidi ya Iran ambavyo ni kinyume cha sheria na vinakiuka ubinadamu,  vimezuia kufikiwa ustawi kamili wa kiuchumi, kijamii na haki za kimsingi za binadamu ikiwa ni pamoja na uhai, afya na ajira."

Katibu wa Idara ya Haki za Binadamu katika Vyombo vya Mahakama vya Iran aidha amebainisha kuhusu mafanikio ya Iran katika uga wa haki za binadamu huku akikosoa hatua zilizo dhidi ya ubinadamu za Marekani. Ameongeza kuwa heshima kwa binadamu na haki za binadamu si zawadi ya Umoja wa Mataifa au mafanikio ya jamii za Magharibi na Ulaya bali ni sehemu ya mantiki ya Iran na chimbuko lake ni Uislamu.

Ikumbukwe kuwa mnano Mei 2018, Rais Donald Trump wa Marekani alichukua uamuzi ulio kinyume cha sheria za kimataifa na kujiondoa katika mapatano ya nyuklia ya Mpango Kamili wa Pamoja wa Utekelezaji (JCPOA) na punde baada ya hapo akatangaza vikwazo dhidi ya Iran.

Baada ya mwaka mmoja wa subira ya kistratijia na kutotimizwa matarajio yake, mnamo Mei 2019 Jamhuri ya Kiislamu ya Iran ilianza kupunguza utekelezaji wa baadhi ya ahadi zake katika mapatano ya JCPOA. Hadi sasa Iran imechukua hatua nne kupunguza utekelezaji wa ahadi zake katika JCPOA.

Tags