Zarif: Natumai ulimwengu wa Kiislamu utapata ushindi dhidi ya maadui
Waziri wa Mambo ya Nje wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran ameeleza matumaini yake kuwa ulimwengu wa Kiislamu utaibuka na ushindi dhidi ya maadui.
Mohammad Javad Zarif amesema hayo katika ujumbe wake alioutuma kwenye ukurasa wake wa Twitter Jumapili ambapo pia ameutakia kheri na fanaka ulimwengu wa Kiislamu kwa mnasaba wa sikukuu ya Idul-Fitr inayodhimishwa hii leo kote duniani.
Amesisitiza kuwa, taifa la Palestina litapata ushindi dhidi ya uvamizi wa utawala ghasibu wa Israel, na Iran ya Kiislamu itapata ushindi dhidi ya vikwazo vya kidhalimu vya Marekani.
Waziri wa Mashauri ya Kigeni wa Iran amebainisha kuwa, "kwa mnasaba wa Iddi yenye baraka, tunamuomba Mwenyezi Mungu alipe ushindi taifa hili la Kiislamu linaloelekea katika kilele cha umoja, izza, na heshima; na linaloelekea kwenye mfumo unaonawiri wa ustaarabu wa kibinadamu."
Dakta Zarif amebainisha kuwa, "tuna imani kubwa na uwezo wa taifa hili na kujitolea muhanga watu wake, na ndani ya siku zijazo, litasherehekea ushindi dhidi ya ukaliaji wa mabavu wa ardhi (za Palestina) na vikwazo vya kidhalimu."