Velayati: Tutalipa kisasi kwa Marekani cha mauaji ya kigaidi ya Qassem Soleimani
Mshauri wa Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu katika masuala ya kimataifa amesema kuwa, kuuawa shahidi Luteni Jenerali Qassem Soleimani ilikuwa jinai kubwa zaidi ya Marekani dhidi ya Iran baada ya Mapinduzi ya Kiislamu na kueleza kwamba, Iran italipa kisasi kwa mauaji hayo na hilo halina shaka.
Dakta Akbar Velayati sambamba na kubainisha kwamba, Marekani ndio adui mkubwa kabisa wa Iran na nchi za Asia Magharibi amesema kuwa, Wamarekani walimuua mgeni rasmi wa serikali ya Baghdad ndani ya ardhi ya Iraq.
Aidha amesema, Jamhuri ya Kiislamui ya Iran haitafumbua macho na kuacha mauaji hayo ya kigaidi dhidi ya Luteni Jenerali Qassem Soleimani yapite hivi hivi, kama ambavyo Iraq nayo pia haitasamehe jinai hiyo kwani tukio hilo ni tusi na udhalilishaji mkubwa kwa Wairaqi na serikali yao yenye nguvu na mamlaka kamili.
Mshauri wa Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu katika masuala ya kimataifa ameashiria muswada wa Bunge la Iraq unaotaka kufukuzwa nchini humo majeshi vamizi ya Marekani na kusema kuwa, anataraji uamuzi huo utatekelezwe haraka iwezekanavyo.
Januari 3 mwaka huu, jeshi la kigaidi la Marekani kwa amri ya rais wa nchi hiyo Donald Trump lilimuua kigaidi Luteni Jenerali Qassem Soleimani, aliyekuwa Kamanda wa Kikosi cha Quds cha Jeshi la Walinzi wa Mapinduzi ya Kiislamu ya Iran (SEPAH) na Abu Mahdi al-Mohandes, Naibu Mkuu wa Harakati ya Wananchi ya Hashdu al-Shaabi pamoja na watu waliokuwa wamendamana nao karibu wa Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Baghdad akiwa mgeni rasmi wa serikali ya Iraq.