Salami: Kikosi cha Majini cha IRGC kina uwezo wa kujibu haraka chokochoko
Kamanda Mkuu wa Jeshi la Walinzi wa Mapinduzi ya Kiislamu (IRGC) amesema kikosi cha baharini cha jeshi la SEPAH kimefikia upeo wa juu wa uwezo wa kujibu haraka tishio lolote la maadui.
Brigedia Jenerali Hossein Salami alisema hayo jana Ijumaa alipovitembelea vikosi vya majini vya IRGC katika visiwa vya Ghuba ya Uajemi na Lango Bahari la Hormuz na kuongeza kuwa, maadui wanapaswa kudiriki uhalisia juu ya uwezo mkubwa wa kujihami na kujibu mapigo wa Jamhuri ya Kiislamu.
Jenerali Salami amebainisha kuwa, "kwa kutumia mifumo ya kisasa ya kielektroniki ya kivita, kikosi cha majini cha IRGC kimeweza kudhibiti kikamilifu jografia yote ya eneo la Ghuba ya Uajemi na Lango Bahari la Hormuz."
Kamanda Mkuu wa SEPAH ameeleza bayana kuwa, kikosi cha baharini cha Jeshi la Walinzi wa Mapinduzi ya Kiislamu kimefanikiwa kupata mafanikio makubwa na hususan katika uzalishaji wa manowari za aina yake, droni za kisasa na makombora ya baharini yanayoelekezwa kutoka mbali,
Brigedia Jenerali Hossein Salam amesema kikosi cha baharini cha jeshi la SEPAH kimeweza kupata mafanikio hayo yote katika kipindi cha miaka mitatu iliyopita.
Kamanda Salami ameongeza kuwa, "maadui wanapaswa kudiriki ukweli wa mambo, kuhusu uwezo mkubwa wa kujilinda na kushambulia wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran na jeshi la IRGC."