UN yataka kusaidiwa mfumo wa afya wa Ukanda wa Gaza
Msemaji wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa amebainisha wasiwasi wake kuhusu hujuma ya Israel katika hospitali ya Kamal Adwan kaskazini mwa Ukanda wa Gaza na kutaka kusaidia mfumo wa matibabu katika eneo hilo.
Stephanie Tremblay Msemaji wa Antonio Guterres Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa amesema anatiwa wasiwasi na mashambulizi mtawalia ya utawala wa Kizayuni katika maeneo mbalimbali ya Gaza na shambulio dhidi ya hospitali ya Kamal Adwan huko kaskazini mwa Ukanda wa Gaza.
Msemaji wa Katibu Mkuu wa UN ameongeza kuwa: Viongozi wa Israel wanapinga juhudi za kimataifa kwa ajili ya kuyafikia maeneo ya kaskazini mwa Gaza.
Tremblay pia ametoa wito wa kuendelea kuheshimiwa sheria na kulindwa wafanyakazi wa sekta ya tiba na vituo vya afya.
Wanajeshi wa utawala wa Kizayuni wamelichoma moto jengo la hospitali ya Kamal Adwan baada ya kutekeleza jinai za kutisha katika maeneo ya hospitali hiyo na kuwauwa shahidi Wapalestina 50 wakiwemo wafanyakazi 5 wa hospitali hiyo.
Wakati huo huo, Harakati ya Mapambano ya Kiislamu ya Palestina Hamas imeitaja jinai hiyo ya kivita ya utawala wa Kizayuni ambayo imetekelezwa kwa ushirikiano kamili wa Marekani na utawala wa Kizayuni huku jamii ya kimataifa ikisalia kimya bila ya kuchukua hatua yoyote dhidi ya utawala wa Kizayuni.