Umoja wa Mataifa: Wapalestina 19 wameuawa shahidi tangu kuanza mwaka huu
Ofisi ya Uratibu wa Masuala ya Kibinadamu ya Umoja wa Mataifa (OCHA) katika ardhi za Palestina zinazokaliwa kwa mabavu imetangaza kuwa, Wapalestina 19 wameuawa shahidi tangu ulipoanza mwaka huu wa 2017.
Taarifa ya ofisi hiyo imeeleza kuwa, Wapalestina wote hao wamekufa shahidi kwa kupigwa risasi na wanajeshi wa utawala haramu wa Israel.
Kwa mujibu wa ripoti hiyo ni kuwa, Wapalestina sita kati ya hao 19 waliouawa shahidi kwa kupigwa risasi ni watoto wadogo.
OCHA imeeleza kuwa, Wapalestina 64 wakiwemo watoto wadogo 11 wamejeruhiwa kwa risasi na wanajeshi wa utawala vamizi wa Israel katika maeneo mbalimbali ya ardhi za Palestina zinazokaliwa kwa mabavu.
Sehemu nyingine ya ripoti ya Ofisi ya Uratibu wa Masuala ya Kibinadamu ya Umoja wa Mataifa (OCHA) katika ardhi za Palestina zinazokaliwa kwa mabavu imeeleza kuwa, milango 25 ya nyumba za Wapalestina imebomolewa na utawala haramu wa Israel katika maeneo mbalimbali ya Ukingo wa Magharibi wa Mto Jordan.
Licha ya kuweko jinai tofauti zinazofanywa na utawala ghasibu wa Israel katika maeneo mbalimbali ya Palestina yakiwemo ya Ukanda wa Gaza, hadi sasa Umoja wa Mataifa haujachukua hatua yoyote ya maana na ya kivitendo kwa ajili ya kuhitimisha jinai hizo za Israel.