Yemen: Trump na washirika wake wanahusika na mauaji al Hudaydah
Mkuu wa Kamati Kuu ya Mapinduzi ya Yemen amesema kuwa Rais Donald Trump wa Marekani, Saudi Arabia na Imarati wanahusika na mauaji ya wakazi wa mji wa al Hudaydah.
Muhammad Ali al Houthi amaeshiria jinai zinazofanywa na muungano vamizi katika mji wa al Hudaydah huko Yemen na kusisitiza kuwa jinai hizo ni jitihada zisizo na matumaini kwa ajili ya kupotosha fikra na mitazamo ya walimwengu kuhusu vitendo vya waziwazi vinavyofanywa na muungano huo vamizi kama kukiuka sheria za kimataifa, kuanzisha vita vya kiuchumi na kuiwekea Yemen mzingiro wa kidhulma.
Al Houthi amesisitiza kuwa wananchi wa Yemen katu hawatasalimu amri mbele ya uvamizi na chokochoko za Marekani, Saudia na Imarati na kwamba wanajeshi vamizi wamewavamia wafungwa wa Kiyemen na kisha kuwatesa na kukiuka haki zao na pia kuwaua watoto, wanawake na raia wa nchi hiyo.
Wakati huo huo televisheni ya al Arabiya imeripoti kuwa serikali ya Marekani imeikabidhi Riyadh ndege kumi za kivita za kisasa licha ya Saudia kuendelea kutekeleza jinai mbalimbali dhidi ya wananchi wa Yemen. Ndege za kivita za Saudi Arabia jana usiku ziliushambulia mji wa al Hudaydah magharibi mwa Yemen na kuuwa watu 15 na kujeruhi zaidi ya 20.