Trump: Saudi Arabia inapasa kuipatia Marekani fedha zaidi
Rais wa Marekani amewaambia viongozi wa utawala wa kifalme wa Saudi Arabia kuwa wanapaswa kulipa gharama za vikosi vya Marekani ambavyo vinailinda nchi hiyo.
Akizungumza katika mkutano wa uchaguzi katika jimbo la Minnesota mbele ya wafuasi wa chama cha Republican, Trump amesema "Sisi tunailinda Saudia hata hivyo wao wanagharamika kidogo katika uwanja huo." Trump amesema utawala wa kifalme wa Saudia unapasa kugharamika pakubwa kutokana na ulinzi unaotolewa na vikosi vya Marekani kwa utawala wa nchi. Amesema amemwambia Mfalme Salman wa Saudia kwamba hawezi kubakia madarakani hata kwa kipindi cha wiki mbili kama hatalindwa na kupewa himaya na Marekani.
Rais wa Marekani aidha ameunga mkono uamuzi uliozusha upinzani wa kuuhamishia ubalozi wa nchi hiyo huko Baitul Muqaddas na kujigamba kwamba yeye ameuhamisha ubalozi wa nchi hiyo huko Quds licha ya kwamba wengi walitaka asichukue hatua hiyo.
Trump alidai kuwa wananchi wa Marekani hivi sasa wana Rais ambaye amesimama imara kwa ajili ya nchi hiyo na kwamba amechukua hatua ambazo hazijawahi kuchukuliwa na rais yoyote aliyetangulia.