Mkuu wa jeshi la Israel akiri wameshindwa kulinda usalama wa Wazayuni
Mkuu wa jeshi la utawala wa Kizayuni wa Israel amekiri kuwa utawala huo umeshindwa katika miezi ya hivi karibuni kuwadhaminia usalama wao walowezi wa Kizayuni wanaishi karibu na Ukanda wa Ghaza.
Kituo cha upashaji habari cha Palestina kimemnukuu Gadi Eizenkot, mkuu wa jeshi la Israel akisema hayo jana na kuongeza kuwa, Israel imekula kipigo kutoka kwa zana ndogondogo tu za Wapalestina wanaoishi Ukanda wa Ghaza.
Vile vile amesema, uwezo wa kijeshi wa vikosi vya muqawama katika Ukanda wa Ghaza ni tatizo kubwa kwa Israel na umewasababishia hali ngumu wakazi wa vitongoji vya walowezi wa Kizayuni.

Hii ni katika hali ambayo Jumamosi usiku, mamia ya Wazayuni wanaoishi mjini Tel Aviv walivaa vizibao vya njano na kushiriki kwa mara ya pili katika maandamano ya kulalamikia hali ngumu ya maisha na ughali wa bidhaa.
Waandamanaji hao walilaani pia siasa za waziri mkuu wa utawala wa Kizayuni, Benjamin Netanyahu na kutaka serikali yake iondolewe mara moja.