Gaidi hatari zaidi atiwa mbaroni kaskazini mwa Iraq
Duru za intelijensia za Iraq zimetangaza habari wa kutiwa mbaroni gaidi hatari mno katika mkoa wa Nainawa (Nineve) wa kaskazini mwa nchi hiyo.
Kwa mujibu wa shirika la habari la Baghdad al Yaum, makachero wa kikosi cha ujasusi wa kijeshi cha Iraq, Ijumaa walifanikiwa kumtia mbaroni gaidi mmoja hatari sana katika eneo liitwalo Zummar la mkoa wa Nainawa ambaye anajulikana kwa jina bandia la Abul Karim.
Afisa mmoja wa masuala ya kiintelijensia wa Iraq ameliambia shirika hilo kwamba gaidi huyo ni miongoni mwa magaidi hatari sana. Ni mwanachama wa genge la kigaidi la 'Ain Jalut linalofanya mashambulizi dhidi ya askari wa Iraq.
Amesema, mara tu baada ya kutiwa mbaroni Abul Karim, amekabidhiwa haraka kwa idara ya ujasusi inayoendesha mapambano dhidi ya magaidi katika eneo la Zummar.
Licha ya magaidi wa Daesh (ISIS) kusambaratishwa nchini Iraq mwezi Disemba 2017 na licha ya kuendelea operesheni mbalimbali za kijeshi na kiusalama za Iraq, lakini bado mabaki ya magaidi hao ambao wamejificha ndani ya jamii, wapo katika maeneo tofauti ya Iraq. Mara kwa mara magaidi hao wanafanya jinai na vitendo vya kigaidi dhidi ya raia na maafisa usalama wa Iraq hasa kaskazini mwa nchi hiyo.
Viongozi wa dola la kibeberu na kiistikbari la Marekani wametangaza mara kadhaa kwamba wao ndio walioliunda genge hilo la kigaidi na kulipandikiza katika nchi za Iraq na Syria.