Matatizo yanayotokana na kutojishughulisha na michezo yameyagharimu mataifa mabilioni ya dola
Watafiti wa masuala ya afya na tiba wamesema matatizo ya afya yaliyosababishwa na watu kutojishughulisha na harakati za michezo katika mwaka 2013 yameyagharimu mataifa dola zipatazo bilioni 67.5.
Kiwango hicho ni zaidi ya Pato Jumla la Ndani (GDP) la nchi nyingi duniani.
Kwa mujibu wa makala iliyoandikwa na jarida moja la tiba, dola bilioni 53.8 kati ya fedha hizo zimetumika kwa ajili ya matunzo ya kiafya na dola bilioni 13.7 zimegharamia matibabu ya viungo vilivyopotea.

Waandishi wa makala hiyo wamesema matokeo ya utafiti huo yametokana na taarifa za kiuchumi na za idadi ya watu za nchi 143 zinazounda asilimia 93 ya watu wote duniani.
Watafiti wa masuala ya afya wanaeleza kuwa mtindo wa maisha wa kutojishughulisha na harakati za michezo unasababisha vifo vya watu zaidi ya milioni tano duniani kila mwaka.
Kwa mujibu wa utafiti huo kutofanya harakati za michezo kwa wananchi wa nchi tajiri duniani kikwaida kumekuwa kukiwagharimu pakubwa kifedha wananchi hao; huki kwa nchi masikini hali hiyo hupelekea kuibuka maradhi na wakati mwingine hata kifo.
Shirika la Afya Duniani WHO linapendekeza kwamba, mtu anapswa kufanya mazoezi kwa muda wa dakika 150 kwa wiki. Hata hivyo, watafiti wa masuala ya afya na tiba walioandika makala hii wao wanapendekeza mtu afanye mazoezi kwa muda wa dakika 60 yaani saa moja kila siku ili aweze kudumisha afya na usalama wa mwili wake.