Shirika la ujasusi la Marekani (CIA) limeingilia chaguzi 81 duniani
Mkuu wa zamani wa Shirika la Ujasusi la Marekani CIA, James Clapper amekiri kwamba shirika hilo limehusika na uingiliaji wa chaguzi 81 kote duniani.
Clapper amesema kuwa katika kipindi cha uhai wake shirika hilo limekuwa likiingilia chaguzi za nchi nyingine kwa kufanya uchakachuaji au kuingilia moja kwa moja au hata kuandaa mazingira ya kuziondoa madarakani serikali mbalimbali. Uchunguzi unaonyesha kwamba, kwa miaka kadhaa madola makubwa hususan Marekani kuanzia mwaka 1946 kufikia 2000, yameingilia chaguzi 117 katika nchi nyingine huku Washington ikiwa ndio inayoongoza katika uwanja huo.
![](https://media.parstoday.ir/image/4bn37145d5bc27xcii_800C450.jpg)
Kwa mujibu wa ripoti hiyo, katika kipindi hicho Shirika la Ujasusi la CIA liliingilia chaguzi 81 katika nchi 47. Nalo Shirika la Habari la Russia Today limetangaza kwamba, viongozi wa Marekani wanadai kuwa serikali ya Russia iliingilia uchaguzi wa nchi hiyo wa mwaka 2016 katika hali ambayo nyaraka zinaonyesha kuwa kwa mara kadhaa White House imekusudia kuingilia masuala ya ndani ya Russia.
![](https://media.parstoday.ir/image/4bpqcda719d3a216dhz_800C450.jpg)
Kwa mujibu wa ripoti hiyo, miongoni mwa uingiliaji huo wa Marekani nchini Russia ni kwamba mwaka 1990 washauri watatu wa Marekani walikuwa wakiongoza kwa siri vyombo vya kampeni vya Boris Yeltsin, rais wa zamani wa nchi hiyo.