Magaidi wanane wa Boko Haram wauawa Nigeria
Jeshi la Nigeria limetangaza kuwa limewauwa wanachama wanane wa kundi la kigaidi la Boko Haram kaskazini mashariki mwa nchi hiyo.
Sani Othman Msemaji wa jeshi la Nigeria ameeleza leo kuwa jeshi hilo limewauwa wanachama wanane wa Boko Haram katika mji wa Gubio katika jimbo la Borno kufuatia oparesheni mpya iliyofanywa na jeshi kaskazini mashariki mwa nchi.
Taarifa ya msemaji wa jeshi la Nigeria imeongeza kuwa jeshi la Nigeria limenasa pia silaha na zana nyingi za kijeshi katika oparesheni hiyo. Wakati huo huo vikosi vya jeshi la Nigeria kwa kushirikiana na brigedi maalumu vilikuwa tayari vimewafurusha wanamgambo wa Boko Haram katika vijiji vinane kaskazini mashariki mwa nchi hiyo, ambapo jeshi hilo sasa linavidhibiti kikamilifu vijiji hivyo. Rais Muhamadu Buhari wa Nigeria alisisitiza hivi karibuni katika Mkutano wa Viongozi wa nchi katika Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa kuhusu mapambano dhidi ya kundi la kigaidi la Boko Haram. Maelfu ya watu wa kaskazini mashariki mwa Nigeria wameuawa katika kipindi cha miaka sita cha kujiri hujuma na mashambulizi ya Boko Haram nchini humo.