Amnesty International yaikosoa Afrika Kusini kwa kushindwa kumkamata al-Bashir
Shirika la kimataifa la kutetea haki za binadamu la Amnesty International limeikosoa serikali ya Afrika Kusini kwa kushindwa kumkamata Rais wa Sudan, Omar Hassan al-Bashir alipoitembelea nchi hiyo mwezi Julai mwaka jana.
Shirika hilo limetoa ripoti yake ya kila mwaka kuhusu hali ya mambo kusini mwa Afrika ambapo imesema Pretoria ilifeli kutekeleza majukumu yake ya kimataifa baada ya kumruhusu al-Bashir kuondoka Afrika Kusini mwezi Julai mwaka jana licha ya kuweko waranti wa kimataifa dhidi ya Rais huyo wa Sudan.
Rais wa Sudan alikuwa Afrika Kusini mwaka uliopita kuhudhuria mkutano wa viongozi wa Afrika uliofanyika mjini Johannesburg. Mahakama moja ya Afrika Kusini ilikuwa imeagiza kukamatwa Rais al-Bashir na kukabidhiwa kwa Mahakama ya Kimataifa ya Makosa ya Jinai (ICC) anakotakiwa kujibu tuhuma za mauaji ya kimbari katika eneo la Darfur na jinai dhidi ya binadamu.
Amnesty international imelitaka Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa kutopuuza suala hilo na kuchukua hatua dhidi ya Afrika Kusini ili mataifa mengine yasifuate mkondo huo.