Drone za Marekani zatumika katika mpaka wa Tunisia, Libya
Rais wa Tunisia ameunga mkono kutumika ndege zisizo na rubani (drone) za Marekani katika mpaka wa nchi yake na Libya.
Rais Beji Caid Essebsi amesema anaunga mkono suala la kutumika ndege zisizo na rubani za Marekani katika operesheni za upepelezi kwenye mpaka wa Tunisia na Libya lakini anapinga kuanzishwa kambi ya kijeshi ya Marekani nchini humo.
Aidha amethibitisha habari kuwa, maafisa 70 wa kijeshi wa Marekani wako nchini Tunisia kwa ajili ya kuwapa mafunzo maafisa wa kijeshi wa Tunisia na ndege zisizo na rubani za Marekani zinatumika katika operesheni za upelelezi kwenye mpaka wa nchi hiyo na Libya.
Kabla ya hapo baadhi ya vyombo vya habari vilikuwa vimeripoti kuwa, Marekani inatumia kambi za kijeshi za Tunisia kufanya operesheni za kijasusi nchini Libya.
Waziri wa Ulinzi wa Tunisia kwa upande wake aliwahi kusema kuwa, nchi yake imepokea baadhi ya vifaa vya kijeshi zikiwemo ndege zisizo na rubani kwa ajili ya kufanya operesheni za kijasusi na kukabiliana na harakati zozote zile zisizo za kawaida. Mfumo huo wa kijeshi unajumuisha ndege na magari kadhaa ya deraya.