Rais Salva Kiir atoa amri ya kupambana na vitisho vya waasi
Rais Salva Kiir wa Sudan Kusini amesisitizia udharura wa kukabiliana na vitisho vya makundi ya upinzani vinavyohatarisha usalama wa nchi hiyo.
Rais Salva Kiir aliyasema hayo jana ambapo sanjari na kuashiria ongezeko la makundi ya waasi, ametaka kufanyika operesheni kali ya kuisafisha Sudan Kusini kutokana na hatari hiyo. Amesisitiza kuwa, mapambano ya dhati ya serikali yake dhidi ya makundi ya waasi ndio kipaumbele kikuu kwa jeshi la nchi. Kwa mujibu wa ripoti hiyo, kufuatia ongezeko la machafuko katika eneo, polisi wa Sudan Kusini inatakiwa kufanya juhudi kubwa kwa ajili ya kupambana na makundi ya namna hiyo yanayohatarisha usalama na amani ya nchi.
Katika fremu hiyo msemaji wa Rais Kiir sambamba na kuunga mkono amri mpya ya rais huyo kwa ajili ya kukabiliana na makundi ya upinzani wa serikali, ametaka maelewano ya kisiasa na nchi jirani ya Sudan kwa ajili ya kukabiliana na tatizo hilo. Hayo yanajiri katika hali ambayo, hivi karibuni kuliripotiwa kujiri mauaji dhidi ya watu 25 na wengine 17 kujeruhiwa, katika mfululizo wa mashambulizi ya kundi moja lililojitenga na lenye mafungamano na Riek Machar, huko mashariki mwa Sudan Kusini. Kwa mujibu wa ripoti hiyo wakazi wa eneo hilo wamepatwa na wasi wasi mkubwa na kuwafanya kukimbia makazi yao.