Askari waasi wa Côte d’Ivoire wamuachilia huru Waziri wa Ulinzi
Askari waasi wa Côte d’Ivoire wamemuachilia huru Waziri wa Ulinzi wa nchi hiyo leo asubuhi, baada ya kumshikilia kwa masaa machache katika makazi yake.
Habari kutoka nchini humo zimeeleza kuwa, askari hao walivamia makazi ya Alain Richard Donwahi, muda mfupi baada ya Rais Alassane Ouattara kutangaza kutupilia mbali makubaliano yaliyotangazwa awali baina ya pande mbili.
Richard Donwahi alitiwa nguvu na kundi la askari hao katika mji wa Bouaké alikokuwa ameenda kwa ajili ya kufanya mazungumzo na askari hao, ambapo baada ya kutekwa alizuiliwa kutoka mjini hapo. Askari hao walianzisha wimbi la machafuko siku ya Ijumaa katika kulalamikia mishahara yao ambapo sanjari na kuasi walivamia ghala la silaha katika mji huo na kuanza kufyatua ovyo risasi. Kadhalika askari hao waliudhibiti mji huo wenye watu wanaokadiriwa kuwa laki tano. Jumamosi ya jana Rais Alassane Ouattara alitangaza habari ya kufikiwa makubaliano kati ya serikali na kundi la askari hao kwa ajili ya kuhitimisha hali ya machafuko nchini humo.
Rais huyo alitangaza kuwa, alikuwa tayari kuwaongezea mishahara askari hao sanjari na kuwadhaminia makazi na kuinua maisha yao. Hata hivyo askari hao walitupilia mbali makubaliano hayo na Rais Alassane Ouattara kwa madai kwamba yalikuwa hayatoshi. Mji wa Bouaké ulidhibitiwa na waasi mwaka 2002 hadi 2011 wakati walipofurushwa na jeshi la serikali kutoka mji huo.