Jeshi la Tunisia latumia mizinga kushambulia maficho ya magaidi
Kikosi cha mizinga cha jeshi la wananchi wa Tunisia kimeshambulia maficho ya magaidi kaskazini magharibi mwa nchi hiyo.
Mtandao wa habari ya Zoom Tunisia umetangaza habari hiyo na kuongeza kuwa, kikosi cha mizinga cha jeshi hilo kimefanya mashambulizi hayo leo asubuhi katika milima ya Wargha mkoani Le Kef, kaskazini magharibi mwa nchi hiyo.
Duru nyingine za habari za Tunisia nazo zimetangaza habari hiyo bila ya kuashiria hasara zilizosababishwa na shambulizi hilo la mizinga.
Wizara ya Mambo ya Ndani ya Tunisia wiki iliyopita ilitoa tamko na kusema kuwa, imefanikiwa kugundua na kusambaratisha magenge mawili ya kigaidi na kwamba polisi wa nchi hiyo wamewatia mbaroni magaidi 11 katika mikoa miwili ya mashariki mwa nchi hiyo.
Hivi sasa Tunisia ni moja ya nchi ambazo raia wake wengi wamejiunga na makundi ya kigaidi katika nchi za nje. Inakisiwa kwamba, kuna karibu raia elfu tano wa Tunisia waliojiunga na magenge ya kigaidi nje ya nchi hiyo.