Afrika Kusini kusaini mikataba ya ujenzi wa vituo vya umeme wa nyuklia
Afrika Kusini inatazamiwa kusaini mikataba mipya na yenye uwazi na nchi tano kuhusu ujenzi wa vituo vya kuzalisha umeme wa nyuklia.
Wizara ya Nishati ya Afrika Kusini imesema imechukua hatua hiyo baada ya mahakama ya nchi hiyo kubatilisha mkataba uliokuwa umetiwa saini na Russia kwa msingi wa kukosekana uwazi katika suala la ushuru. Kwa msingi huo serikali ya nchi hiyo imeamua kuandaa mikataba mipya na Russia, Ufaransa, China, Korea Kusini na Marekani kwa lengo la kujenga vituo vya umeme wa nyuklia vinavyotazamiwa kugharimu dola bilioni 30 hadi 70.
Wataalamu wa masuala ya uchumi wanasema Afrika Kusini haina uwezo wa kugharamia miradi hiyo huku wapinzani wa Rais Jacob Zuma wakisema mikataba hiyo ni chimbuko la ufisadi. Hata hivyo Zuma amekanusha madai hayo.
Shirika la Kitaifa la Nishati Afrika Kusini Eskom linasema nishati ya nyuklia inaweza kuwa na nafasi muhimu katika uchumi wa nchi hiyo ambayo hutegemea sana mkaa wa mawe kuzalisha umeme.