Kesi ya watuhumiwa 26 wa ugaidi yasikilizwa nchini Tunisia
Mahakama moja nchini Tunisia imesikiliza kesi ya watuhumiwa 26 wa mashambulizi ya kigaidi yaliyowalenga watalii nchini humo.
Jana Ijumaa ilikuwa siku ya kwanza ya kusikikilizwa hadharani kesi inayowakabili watu 26 wanaotuhumiwa kuhusika katika shambulio la kigaidi dhidi ya watalii mwaka 2015 na kupelekea makumi ya watu kuuawa. Kesi hiyo imesikilizwa mbele ya wanadiplomasia wa Uingereza na chini ya ulinzi mkali sana.
Sita kati ya watuhumiwa hao ni maafisa wa polisi wa Tunisia ambao wanatuhumiwa kufanya uzembe kazini.
Shambulio la kigaidi la mwaka 2015 nchini Tunisia, liliua watalii 38 wa kigeni wakiwemo watalii 30 wa Uingereza katika bandari ya El Kantaoui. Mtu aliyefanya shambulio hilo alipigwa risasi na kuuawa na polisi.
Kundi la kigaidi la Daesh (ISIS) lilitangaza kuhusika na shambulio hilo ambalo liliitia kwenye mgogoro mkubwa sekta ya utalii ya nchi hiyo ya kaskazini mwa Afrika.