Kenya yaimarisha usalama wa wanaoendesha vita dhidi ya mafisadi
https://parstoday.ir/sw/news/africa-i47540-kenya_yaimarisha_usalama_wa_wanaoendesha_vita_dhidi_ya_mafisadi
Serikali ya Kenya imemarisha usalama wa waendesha mashtaka, makachero na mashahidi wanaohusika katika kampeni mpya rasmi ya vita dhidi ya mafisadi nchini humo.
(last modified 2023-11-27T12:14:11+00:00 )
Aug 19, 2018 07:21 UTC
  • Kenya yaimarisha usalama wa wanaoendesha vita dhidi ya mafisadi

Serikali ya Kenya imemarisha usalama wa waendesha mashtaka, makachero na mashahidi wanaohusika katika kampeni mpya rasmi ya vita dhidi ya mafisadi nchini humo.

Kwa mujibu wa ripoti ya gazeti la Sunday Nation,  serikali imechukua hatua maalumu kuimarisha usalama wa  Mwendesha Mashtaka Mkuu  (DPP) Noordin Haji ambaye anaongoza vita dhidi ya maafisa wa ngazi za juu serikalini ambao wamehusishwa na ufisadi.

Taarifa zinasema sasa ameongezewa idadi ya walinzi na ni vigumu kufika katika ofisi yake kutokana na hatua kali za usalama zilizochukuliwa.

Aidha Mkurugenzi wa Upelelezi wa Jinai (DCI) George Kinoti na makachero wengine wameongezewa walinzi.

Mwendesha Mashtaka Mkuu  Kenya, (DPP) Noordin Haji

Akizungumza Jumamosi, Rais Uhuru Kenya ameihakikishia Tume ya Kupambana na Ufisadi (EACC) anaiunga mkono kikamilifu katika vita vyake dhidi ya ufisadi. Ametoa wito kwa maafisa wote husika kuimarisha mikakati ya kukabiliana na mafisadi na jinai za kiuchumi nchini humo. Aidha ametaka taasisi zote husika za serikali zishirikiane ili kufanikisha vita dhidi ya ufisadi.