Machar, Mkuu wa waasi Sudan Kusini aapishwa kuwa makamu wa rais
https://parstoday.ir/sw/news/africa-i5857-machar_mkuu_wa_waasi_sudan_kusini_aapishwa_kuwa_makamu_wa_rais
Kiongozi wa waasi Sudan Kusini Riek Machar amewasili katika mji mkuu wa nchi hiyo, Juba na kuapishwa kuwa makamu wa rais wa nchi hiyo.
(last modified 2023-11-27T08:44:11+00:00 )
Apr 26, 2016 10:01 UTC
  • Machar, Mkuu wa waasi Sudan Kusini aapishwa kuwa makamu wa rais

Kiongozi wa waasi Sudan Kusini Riek Machar amewasili katika mji mkuu wa nchi hiyo, Juba na kuapishwa kuwa makamu wa rais wa nchi hiyo.

Machar ameapishwa kuwa makamu wa rais katika serikali inayoongozwa na hasimu wake wa muda mrefu, Rais Salva Kiir. Machar alichelewesha kuwasili Juba kwa miezi kadhaa jambo ambalo liliikasirisha jumuiya ya kimataifa ambayo imehusika katika kuwaleta mahasimu hao wawili pamoja ili wagawane madaraka katika nchi hiyo changa zaidi duniani.

Vita vya ndani nchini humo vilivyoanza Disemba 2013 vimesababisha mauaji ya maelfu ya watu na kulazimisha mamilioni ya wengine kuwa wakimbizi. Nchi hiyo ilitumbukia katika vita vya ndani baada ya Rais Salva Kiir kutoka kabila la Dinka kumtuhumu makamu wake za zamani, Riek Machar wa kabila la Nuer kwamba alihusika na jaribio la kupindua serikali yake.

Kwa mujibu wa mapatano ya amani yaliyotiwa saini Addis Ababa Ethiopia, kutakuwa na serikali ya mpito itakayodumu kwa muda wa miezi 30. Kiir atachukua asilimia 53 ya viti serikalini huku upande wa Machar ukipata asilimia 33 na wafungwa wa zamani wa kisiasa na vyama vingine vya kisiasa vikipata asilimia 7 kila mmoja.