Wanamgambo wa Haftar: Tumeua askari 40 wa Serikali ya Libya
Wanamgambo wanaojiita Jeshi la Taifa la Libya wanaoogozwa na jenerali muasi Khalifa Haftar wanadai wametekeleza operesheni kali iliyoua askari 40 wa Jeshi la Serikali ya Mwafaka wa Kitaifa inayoongozwa na Waziri Mkuu, Fayez al-Sarraj.
Wanamgambo hao wamesema katika taarifa jana Jumanne kuwa, "asubuhi ya leo (jana Jumanne) kundi la waasi (Jeshi la Serikali ya Mwafaka wa Kitaifa) wamejaribu kufanya shambulizi la kioga dhidi ya uwanja wa ndege wa kijeshi wa Watya, yapata kilomita 140 kusini magharibi mwa mji mkuu Tripoli, chini ya himaya ya jeshi la anga la Uturuki, lakini tukajibu mapigo na kuua 40 miongoni mwao, mbali na kujeruhi na kuwatia mbaroni wengine wengi."
Mohamed Gonono, Msemaji wa Jeshi la Serikali ya Mwafaka wa Kitaifa ya Libya amesema askari wao wanaoungwa mkono na jamii ya kimataifa walitekeleza operesheni dhidi ya uwanja wa ndege wa kijeshi wa Watya na kuangamiza idadi kubwa ya wapiganaji wa Khalifa Haftar.
Jenerali Haftar anayeungwa mkono na nchi za Saudi Arabia, Misri, Umoja wa Falme za Kiarabu (Imarati) na baadhi ya nchi za Magharibi, hivi karibuni alitangaza kuvunja makubaliano yaliyofikiwa tarehe 17 Disemba 2015 katika mji wa Skhirat Morocco, yaliyounda Serikali ya Mwafaka wa Kitaifa chini ya usimamizi wa Umoja wa Mataifa
Tangu mwezi Aprili 2019 alianzisha vita vikubwa dhidi ya mji mkuu Tripoli kwa shabaha ya kuuteka na kuivunja Serikali ya Mwafaka wa Kimataifa inayotambuliwa kimataifa. Hata hivyo ndoto za jenerali huyo muasi zimeshindwa kutimia kutokana na muqawama wa Serikali ya Mwafaka wa Kitaifa inayotambulika kimataifa.