Polisi ya Burundi yatangaza idadi ya wahanga wa machafuko ya nchi hiyo
Machafuko nchini Burundi yaliyodumu kwa mwaka mzima sasa yamepelekea watu 451 kuuawa.
Shirika la habari la Xinhua limelinukuu jeshi la polisi la Burundi likitangaza leo kuwa, mgogoro wa kisiasa wa nchi hiyo ulioanza mwezi Aprili 2015 umeshapelekea watu 451 kuuawa na wengine 757 kujeruhiwa.
Baadhi ya watu waliojeruhiwa katika machafuko hayo ni askari polisi wa nchi hiyo.
Kwa mujibu wa ripoti hiyo, maafisa 59 wa polisi wamefungwa jela kwa kutumia nguvu kupita kiasi katika kukabiliana na waandamanaji.
Watu 437 wengine wametiwa mbaroni kwa tuhuma za kufanya maandamano na wamekabidhiwa kwa vyombo vya mahakama.
Tangu mwezi Aprili 2015 Burundi ilitumbukia kwenye machafuko baada ya chama tawala cha CNDD FDD kumuidhinisha Rais Pierre Nkurunziza kugombea urais kwa mara ya tatu mfululizo.
Mbali na wahanga hao, hadi hivi sasa wananchi laki mbili wa Burundi wamelazimika kukimbilia nchi jirani.