EU: Sheria ya Mtandao nchini Tanzania, ifanyiwe marekebisho
https://parstoday.ir/sw/news/africa-i8344-eu_sheria_ya_mtandao_nchini_tanzania_ifanyiwe_marekebisho
Ujumbe wa waangalizi wa uchaguzi wa Umoja wa Ulaya (EU-EOM), umewasilisha ripoti yake kamili yenye mapendekezo tofauti kuhusiana na marekebisho ya kuboresha mchakato mzima wa uchaguzi nchini Tanzania.
(last modified 2023-11-27T08:44:11+00:00 )
Jun 02, 2016 11:23 UTC
  • EU: Sheria ya Mtandao nchini Tanzania, ifanyiwe marekebisho

Ujumbe wa waangalizi wa uchaguzi wa Umoja wa Ulaya (EU-EOM), umewasilisha ripoti yake kamili yenye mapendekezo tofauti kuhusiana na marekebisho ya kuboresha mchakato mzima wa uchaguzi nchini Tanzania.

Mwangalizi Mkuu wa Ujumbe wa Waangalizi wa Uchaguzi wa EU, Bi. Judith Sargentini amesema kuwa, licha ya uchaguzi wa Oktoba 25, 2015 nchini Tanzania kuonyesha kuwa na dhamira ya Watanzania katika kuzingatia mfumo wa kikatiba na kuheshimu misingi ya demokrasia, bado kulikuwepo na kasoro kadhaa kwenye uchaguzi huo. Aidha umetoa mapendekezo kadhaa ikiwa ni pamoja na kuwepo haki ya wagombea binafsi kuweza kugombea katika uchaguzi wowote, kuruhusu haki ya kupinga matokeo ya uchaguzi wa rais kisheria, haki ya vyama vya siasa kuunda umoja wa kiuchaguzi, kuangaliwa upya Sheria ya Makosa ya Mtandao ya mwaka 2015, kuendelezwa muundo wa kudumu wa Tume ya Uchaguzi nchini Tanzania NEC katika ngazi za mikoa. Aidha EU imependekeza kufanyika mchakato wa uteuzi wa makamishna wa uchaguzi wa tume za NEC na ZEC na kadhalika kuangaliwa upya mchakato wa uandikishaji wa majina ya wapiga kura nchini humo hususan Zanzibar ili kutoa fursa ya ushirikishi zaidi na imani ya wapiga kura. Kuhusu Zanzibar, Bi. Judith Sargentini amesema kuwa, licha ya tamko lao la awali kuelezea juu ya wasiwasi wao mkubwa na kuiomba Tume ya Uchaguzi Zanzibar (ZEC) iwasilishe ushahidi wa kuhalalisha uamuzi wa kufuta matokeo ya awali ya uchaguzi wa Oktoba 25 mwaka jana, hadi sasa tume hiyo bado haijafanya hivyo.