Iran yalaani hujuma ya kigaidi dhidi ya ubalozi wa Ujerumani
Jamhuri ya Kiislamu ya Iran imelaani vikali shambulizi la kigaidi lililolenga ubalozi mdogo wa Ujerumani nchini Afghanistan.
Bahram Qassemi, msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje wa Iran amesema kuwa, jamii ya kimataifa inapaswa kuchukua hatua za uhakika kukabiliana na jinamizi la ugaidi.
Amesema kuwa, hujuma kama hiyo iliyolenga ubalozi wa Ujerumani katika mkoa wa Balkha nchini Afghanistan Alkhamisi iliyopita ni dhihirisho tosha kuwa suala la ugaidi linahitaji nguvu za pamoja za nchi zote.
Sambamba na kutoa mkono wa pole kwa jamaa na marafiki wa waathirika wa shambulio hilo na taifa la Afghanistan kwa ujumla, Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje wa Iran amesema ugaidi hautambui taifa, dini wala eneo lolote.
Watu zaidi ya 100 waliuawa na kujeruhiwa katika hujuma hiyo iliyolenga ubalozi mdogo wa Ujerumani katika mji wa Mazar-i-Sharif nchini Afghanistan Alkhamisi iliyopita.