Iran yalaani shambulizi la kigaidi Chabahar, yasema wahusika na mabwana zao watakiona
Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Iran amelaani vikali shambulizi la kigaidi lililofanyika jana Alkhamisi katika mji wa Cahabah huko kusini mashariki mwa Iran.
Gaidi aliyekuwa mmoja alishambulia kituo cha jeshi la polisi katika wilaya ya Chabahar mkoani Sistan na Baluchistan na kulipua gari lililokuwa limesheheni mabomu mbele ya kituo hicho. Polisi wawili wameuawa shahidi katika shambulizi hilo la kigaidi na watu wengine 28 wamejeruhiwa. Gaidi huyo pia ameangamia.
Baada ya shambulizi hilo msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Iran, Bahram Qassemi amesema kuwa, magaidi waliopewa mafunzo katika baadhi ya nchi zinazotambuliwa kuwa vituo vya kulea na kueneza ugaidi na misimamo ya kufurutu mipaka wamefanya tena kitendo hicho cha shari na dhidi ya binadamu katika eneo la kiuchumi la Chabahar kwa shabaha ya kukwamisha ustawi wa kiuchumi na ushirikiano wa Iran na nchi nyingine unaofanyika kwa lengo la kuimarisha usalama na amani ya maeneo ya mpakani.
Qassemi amesisitiza kuwa, magaidi waliohusika na uhalifu huo na mabwana zao watalipa gharama kubwa popote pale walipo kutokana na uhalifu na jinai hiyo.