Iran hufanya majaribio zaidi ya 40-50 ya makombora kila mwaka
Kamanda wa Kitengo cha Angani cha Jeshi la Walinzi wa Mapinduzi ya Kiislamu, IRGC, amezungumzia habari kuhusu Iran kufanya jaribio la kombora la balistiki hivi karibuni na kusema: "Kauli za wakuu wa Marekani ni ishara kuwa, wanalipa umuhimu mkubwa sana suala la majaribio hayo."
Brigedia Jenerali Amir Ali Hajizadeh, Kamanda wa Kitengo cha Angani cha IRGC ameongeza kuwa: "Kila mwaka Iran hufanya majaribio 40 hadi 50 ya makombora.
Disemba Mosi, Mike Pompeo Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani alidai katika ukurasa wake wa Twitter kuwa, Iran hivi karibuni ilifanyia majaribio kombora la balisitiki la masafa ya wastani ambalo lina uwezo wa kubebe vichwa kadhaa.
Siku moja baada ya madai ya Pompeo, Brigedia Abul Fazl Shekarchi, Msemaji wa Majeshi ya Iran alisema kufanya majaribio ya makombora na majaribio mengine ya uwezo wa kujihami Jamhuri ya Kiislamu ya Iran ni katika fremu ya sera za ulinzi za kuwa na uwezo wa kumzuia adui na sera hizo zitaendelea kutekelezwa.
Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran, Mohammad Javad Zarif naye katika kujibu matamshi ya wakuu wa Marekani kuhusu miradi ya makombora ya kujihami ya Iran alisema: "Wakuu wa serikali iliyopita na ya sasa ya Marekani wamekiri kuwa, mapatano ya nyuklia ya Iran, JCPOA na azimio nambari 2231 la Baraza la Usalama, halizuii Iran kuwa na makombora ya kujihami."