Zarif: Vikwazo haviwezi kutenganisha wananchi wa Iran na serikali yao
Waziri wa Mashauri ya Kigeni wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran amesema mashinikizo na vikwazo vya Marekani na nchi za Magharibi kwa ujumla vimeshindwa kulipigisha magoti taifa la Iran na kwamba katu njama hizo haziwezi kuwatenganisha Wairani na serikali yao.
Muhammad Javad Zarif ameyasema hayo katika mkutano uliofanyika jana Jumanne hapa Tehran, kuhusu sera za kigeni za Iran, katika kipindi cha miaka 40 ya ushindi wa Mapinduzi ya Kiislamu.
Dakta Zarif ameuambia mkutano huo kwamba, "Kadri wanavyoshadidisha mashinikizo dhidi yetu, ndivyo tunavyozidi kuwategemea wananchi wetu. Sio tu hatuhitaji msaada wa kigeni kujiimarisha katika uga wa usalama, lakini pia ustawi na maendeleo yanayoshuhudiwa hapa nchini yanafanyika kwa kulitegemea taifa letu licha ya mashinikizo."
Amezitaja sera na mashinikizo hayo ya Marekani na waitifaki wake kama siasa zilizoshindwa na kufeli mkabala wa Iran, na kusisitiza kwamba Wairani kamwe hawatasalimu amri.
Mahudhurio makubwa ya mamilioni ya watu katika maadhimisho ya ushindi wa Mapinduzi ya Kiislamu Februari 11 yamewaghadhabisha na kuwatia unyonge viongozi wa Marekani na utawala wa Kizayuni wa Israel.
Dakta Zarif amebainisha kuwa, Marekani imefeli kuiteteresha Iran kupitia njama zake zote katika kipindi chote cha miaka 40 iliyopita.