Mousavi: Utendaji mbovu wa Trump umepelekea wauguzi Marekani wapate mashinikizo
Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Iran amesema utendaji mbovu wa serikali ya Donald Trump ndio chanzo cha mashinikizo makubwa kwa wauguzi nchini Marekani.
Sayyid Abbas Mousavi, Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Iran aliyasema hayo Jumanne katika ujumbe kupitia ukurasa wake wa Twitter kwa mnasaba wa Siku ya Wauguzi Duniani ambayo huadhimishwa Mei 12. Katika ujumbe wake, Mousavi amesema: "Katika zama hizi za janga la COVID-19, watu wote Iran na duniani wana deni kubwa kwa wauguzi ambao wanahatarisha maisha yao kwa ajili ya afya ya wengine."
Mousavi ameashiria kuenea sana ugojwa wa COVID-19 nchini Mareknai na kusema hatari wanayokumbana nayo wauguzi inahisika zaidi nchini Marekani na kuongeza kuwa: "Utendaji mbovu wa serikali ya Trump umepelekea wauguzi wapate mashinikizo yasiyoweza kustahamilika kwani wako mstari wa mbele bila vifaa vya kutosha."
Mei 12 ni Siku ya Wauguzi Duniani na siku hii imetengwa kwa ajili ya kuwawenzi na kuwashukuru wauguzi kutokana na jitihada kubwa wanazofanya katika kazi yao.
Kwa mujibu wa takwimu za hivi karibuni, watu milioni 1.385 wameambukizwa COVID-19 nchini Marekani na wengine karibu 82,000 wamepoteza maisha kutokana na ugonjwa huo hatari. Takwimu hizo zinaifanya Marekani kuwa na idadi kubwa ya wagonjwa waathirika wa COVID-19 duniani.