Washindi wa Tuzo ya Mustafa SAW 2021 watunukiwa zawadi mjini Tehran
https://parstoday.ir/sw/news/iran-i76022-washindi_wa_tuzo_ya_mustafa_saw_2021_watunukiwa_zawadi_mjini_tehran
Wanasayansi watano Waislamu wametunukiwa zawadi ya Tuzo ya Mustafa SAW ya mwanasayansi bora katika Ulimwengu wa Kiislamu mwaka huu wa 2021.
(last modified 2023-11-27T08:44:11+00:00 )
Oct 22, 2021 00:25 UTC
  • Washindi wa Tuzo ya Mustafa SAW 2021 watunukiwa zawadi mjini Tehran

Wanasayansi watano Waislamu wametunukiwa zawadi ya Tuzo ya Mustafa SAW ya mwanasayansi bora katika Ulimwengu wa Kiislamu mwaka huu wa 2021.

Katika sherehe iliyofanyika katika mji mkuu wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran, Tehran jana Alhamisi, washindi hao walitunukiwa zawadi zenye jumla ya thamani ya dola milioni moja.

Sherehe hiyo imehudhuriwa na Makamu wa Kwanza wa Rais wa Iran anayeshughulikia masuala ya Sayansi na Teknolojia Dkt. Sorena Sattari, Waziri wa Sayansi, Utafiti na Teknolojia Iran Muhammad-Ali Zolfigol na Waziri Mkuu wa Zamani wa Iraq Adil Abdul-Mahdi.

Washindi wa tuzo hiyo katika nyanja zote za Sayansi na Teknolojia ni msomi Muirani Profesa Cumrun Vafawa wa Chuo Kikuu cha Harvard kwa kazi yake "F-Theory" na Zahid Hasan kutokana na kazi yake ya "Weyl fermion semimetals." Zahid Hasan mwenye asili ya Bangladesh kwa sasa ni profesa katika Chuo Kikuu cha Princeton huko New Jersey nchini Marekani.

Washindi wa Tuzo ya al Mustafa 2021 kutoka ndani ya nchi za Kiislamu ni Yahya Tayalati kutoka Moroco, Prf. Mohamed H. Sayegh wa Lebanon na Muhammad Iqbal Choudhary wa Pakistan.

Tuzo ya Mustafa hutolewa katika uwanja wa fizikia kwa wanasayansi bora wa Kiislamu ambao wanaishi na kufanya kazi ndani ya nchi za Waislamu na nje ya nchi hizo.

Tuzo hii ya aina yake katika ulimwengu wa Kiislamu  hutolewa na Jamhuri ya Kiislamu ya Iran kila baada ya miaka miwili kwa wasomi na wanasayansi bora wa Ulimwengu wa Kiislamu waliovumbua mambo mbalimbali katika masuala ya elimu na sayansi kwa ajili ya kuboresha maisha ya mwanadamu.

Tuzo ya Sayansi ya Mustafa SAW (The Mustafa (PBUH) Prize) ilizinduliwa mwaka 2013 na kisha ilitolewa mara ya kwanza mwaka 2015 mjini Tehran ambapo wakati huo washindi walikuwa ni Preofesa Omar Yaghi wa Jordan, mtaalamu wa nanoteknolojia na Profesa Jackie Ying wa Singapore katika uga wa bio-nanoteknolojia.