Kiongozi wa Mapinduzi ya Kiislamu: Vikwazo vya michezo vinakadhibisha madai ya Wamagharibi
https://parstoday.ir/sw/news/iran-i89128-kiongozi_wa_mapinduzi_ya_kiislamu_vikwazo_vya_michezo_vinakadhibisha_madai_ya_wamagharibi
Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu amevitaja vikwazo vya michezo baada ya kuanza vita vya Ukraine kuwa vinakadhibisha madai ya waistikbari na wafuasi wao kuhusu kutoingizwa siasa katika michezo.
(last modified 2026-08-03T07:36:50+00:00 )
Oct 10, 2022 07:10 UTC
  • Kiongozi wa Mapinduzi ya Kiislamu: Vikwazo vya michezo vinakadhibisha madai ya Wamagharibi

Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu amevitaja vikwazo vya michezo baada ya kuanza vita vya Ukraine kuwa vinakadhibisha madai ya waistikbari na wafuasi wao kuhusu kutoingizwa siasa katika michezo.

Ayatullah Ali Khamenei aliyasema hayo katika hadhara ya waandalizi wa Kongamano la Mashahidi Wanamichezo na Familia Zao lililofanyika mjini Tehran na kuongeza kuwa: Vikwazo vinavyowekwa katika sekta ya michezo vimeonesha kuwa, Wamagharibi huvuka hata mistari yao myekundu kwa ajili ya kukidhi maslahi yao. 

Amesisitiza udharura wa kuambatana ushindi wa kiufundi na ushindi wa masuala ya kiroho na kimaadili na kusema: "Pale wanamichezo wa Iran wanaponyimwa medali kwa sababu ya kukataa kushindana na wanamichezo wa utawala wa Kizayuni wa Israel kwa hakika huwa wamepata ushindi, kwa sababu kushindana na Wazayuni kuna maana ya kuutambua rasmi utawala ghasibu, katili na unaoua watoto, na ni kukanyaga na kutupilia mbali ushindi wa kimaadili kwa sababu ya kutaka kupata ushindi wa kidhahiri tu, suala ambalo kwa hakika halina thamani yoyote." 

Kongamano la Mashahidi Wanamichezo

Kiongozi wa Mapinduzi ya Kiislamu amesema mazingira ya sasa ya michezo hapa nchini yameathiriwa na hali ya kiroho ya wanamichezo mashahidi waliouawa katika njia ya Mwenyezi Mungu. Ametaja baadhi ya vielelezo vya kushikamana na dini wanamichezo wa Iran na kusema: Mahudhurio ya mwanamichezo wa kike wa Iran kwenye majukwaa ya michuano na mashindano mbalimbali wakiwa wamevalia vazi la hijabu ya Kiislamu, kutopeana mikono na wanaume ajnabi, kusabilia nishani zao za ubingwa kwa familia za mashahidi, kusujudu baada ya kupata ushindi, kutaja majina ya Maimamu watoharifu baada ya ushindi na ushiriki wa ujumbe wa wanamichezo katika ziara ya  Arbaeen, ni matukio ya kustaajabisha na ya kipekee katika dunia ya leo ya kimaada na iliyojaa ufisadi; jambo ambalo linapaswa kupewa mazingatio kwa ajili ya kutambua ipasavyo upeo wa masuala ya kiroho na kimaadili wa taifa la Iran.

Ayatullah Ali Khamenei amewashauri wanamichezo kulinda heshima yao na sifa ya taifa na nchi kwa kuchunga mienendo yao ndani na nje ya medani ya mashindano na kusema: "Awali, mazingira yetu ya michezo yalipambwa kwa jina la Mwenyezi Mungu, Mtume na Maimamu watoharifu na masuala ya kidini na kimaadili, lakini Wamagharibi wamejaribu kuingiza utamaduni wao kwenye michezo mipya; hivyo sambamba na kujifunza na kupiga hatua za maendeleo katika michezo mipya, tunapaswa kutawalisha utamaduni wetu na tusiruhusu michezo kuwa daraja la kuingiza utamaduni wa Kimagharibi."