Iran yapinga madai ya Ukraine kwamba iliipatia Russia ndege zisizo na rubani
Mwakilishi wa kudumu wa Iran katika Umoja wa Mataifa amekanusha madai ya Ukraine kwamba Jamhuri ya Kiislamu ilikiuka azimio la Umoja wa Mataifa kwa kile Kiev inachodai kuwa eti kuipatia Russia ndege zisizo na rubani au drone.
Amir-Saeid Iravani aliyasema hayo katika barua yake kwa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres na Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa (UNSC) siku ya Alhamisi.
Mjumbe huyo aliwasilisha barua hiyo baada ya Balozi wa Ukraine katika Umoja wa Mataifa Sergiy Kyslytsya kuwaandikia barua Guterres na wajumbe wa Baraza la Usalama, akidai kuwa Jamhuri ya Kiislamu "ilikiuka" azimio nambari 2231 la UNSC kutokana na kile alichodai ni kuipa Russia ndege zisizo na rubani.
Barua hiyo ya Ukraine inadai kuwa Iran ilikiuka azimio hilo ambalo linaipiga marufuku Tehran kuuza mifumo ya ndege zisizo na rubani zenye uwezo wa kuruka zaidi ya kilomita 300. Kyslytsya pia aliwaalika wataalamu wa Umoja wa Mataifa kutembelea nchi yake ili kufahamu, kile alichokiita, ndege zisizo na rubani zilizotengenezwa na Iran zinazotumiwa na Russia katika operesheni ya kijeshi.
Akijibu madai ya Ukraine, Iravani alibainisha kuwa vikwazo vilivyotajwa katika azimio hilo la Baraza la Usalama "vilimalizika Oktoba 2020."
Aliongeza kuwa tangu wakati huo, Iran haijakuwa chini ya vikwazo vya , uuzaji au uhamishaji wa silaha kwa nchi zingine.
Aidha amesema Jamhuri ya Kiislamu "haijatoa, wala haina nia ya kutoa vitu, nyenzo, vifaa, bidhaa, na teknolojia zinazochangia uundaji wa silaha za nyuklia."
Mwanadiplomasia hiyo wa Iran ametoa wito kwa katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa kuzuia "matumizi mabaya" yoyote ya azimio hilo kuhusiana na vita vya Ukraine.
Hatimaye alitoa wito kwa chombo hicho cha dunia kukabiliana na madai hayo yasiyo na msingi dhidi ya Iran.