Apr 22, 2024 02:31 UTC

Jumuiya ya Waislamu wa Marekani imetangaza kuwa, rais wa nchi hhiyo Joe Biden atakuwa msaliti kama atasaini msaada mpya wa kijeshi kwa utawala wa Kizayuni unaoua kwa umati watoto wadogo huko Ghaza na atakuwa amevuruga kabisa uhusiano wake na Waislamu.

Hisia kali zilizooneshwa na Jumuiya ya Waislamu wa Marekani kuhusu msaada mpya wa nchi hiyo kwa utawala wa Kizayuni zimetokana na kwamba kila mtu duniani anaona jinsi utawala wa Kizayuni unavyofanya mauaji ya kimbari huko Ghaza Palestina lakini wakati huo huo serikali ya Joe Biden imeamua kuipa Israel msaada mkubwa wa kijeshi kwa madai ya eti kujihami.

Waislamu wa nchini Marekani wamekasirishwa na serikali ya nchi hiyo kutokana na uungaji mkono mkono wake wa pande zote kwa utawala wa Kizayuni kiasi kwamba baadhi ya wabunge Waislamu wa nchi hiyo wamemwambia Joe Biden asitarajie kupata kura za Waislamu katika uchaguzi ujao. 

Misaada ya Marekani inatumiwa na Israel kufanya jinai kama hizi dhidi ya watoto na raia wa kawaida wa Palestina

 

Jumuiya ya Waislamu wa Marekani imemwambia Biden na serikali yake kwamba, kama ataidhini msaada huo kupelekwa kwa utawala wa Kizayuni, hakutabakia nukta yoyote ya kurudi nyuma na ya kubakisha uhusiano baina ya serikali hiyo na Waislamu ambao tayari hivi sasa umeharibika vibaya kutokana na uungaji mkono wa kila upande wa Marekani kwa utawala wa Kizayuni; utawala ambao unaendelea kufanya jinai za kutisha dhidi ya Waislamu wa Palestina hasa wa Ukanda wa Ghaza. 

Baada ya bunge la Marekani kupasisha msaada mpya wa kijeshi wa dola bilioni 26 kwa utawala katili wa Israel, hivi sasa muswada wa msaada huo unasubiri kutiwa saini na rais wa Marekani, Joe Biden wiki ijayo.

Tags