Daesh yasisitiza kuzidisha mashambulizi ya kigaidi katika pembe mbalimbali duniani
Kundi la kigaidi la Daesh limewataka wanachama wake kuendesha mashambulizi ya kigaidi katika maeneo mbalimbali duniani.
Kundi la kigaidi la Daesh jana alasiri lilituma ujumbe mpya wa sauti likiwatolea wito wanachama wake waliopo Marekani, Russia, Australia, Iraq, Syria na Ufilipino kupanga mashambulizi katika mwezi huu Mtukufu wa Ramadhani. Ujumbe huo wa sauti wa Daesh ulitumwa kwa njia ya Telegram jana Jumatatu ambapo inaonekana kuwa sauti iliyorekodiwa kwenye mkanda huo ni ya Abu Hassan al Muhajer Msemaji Rasmi wa kundi hilo la kigaidi.
Msemaji huyo gaidi amewataka wanachama wa Daesh katika nchi hizo na kwingineko kuendesha mashambulizi dhidi ya wale aliowataja kuwa ni maadui wa kundi hilo.