Kombora la Yemen laua mamluki 35 wa Saudia mkoani Taizz
Vikosi vya Yemen vimefyatua kombora la balestiki na kuangamiza makumi ya mamluki wa Saudi Arabia katika mkoa wa Taizz, kusini mashariki mwa nchi.
Duru za kijeshi zimeiambia televisheni ya al Masira kuwa, vikosi vya Yemen vilifyatua kombora hilo aina ya Qaher 2-M jana alasiri kuelekea katika kambi ya mamluki hao mjini al Khayami.
Habari zinasema kuwa, mamluki 35 wameuawa huku wengine zaidi ya 20 wakijeruhiwa.
Kutokana na hasira za kuuawa mamluki wake, jeshi la Saudia baadaye jana lilitekeleza mashambulizi ya anga katika wilaya ya Sahar mkoani Sa'ada na kuua watu watatu wa familia moja.
Wiki iliyopita, Jeshi la Yemen liliushambulia kwa kombora uwanja wa ndege wa Jizan, kusini magharibi mwa Saudia ikiwa ni katika hatua ya ulipizaji kisasi kutokana na uvamizi wa Saudia na washirika wake dhidi ya taifa hilo la Kiarabu, tangu Machi mwaka 2015.
Licha ya Saudia kuua watu zaidi ya elfu 13 katika mashambulizi hayo, lakini imeshindwa kufikia malengo yake machafu.