Katibu Mkuu wa Hizbullah: Ni ujuha na ujinga kuiamini Marekani
Katibu Mkuu wa Harakati ya Mapambano ya Kiislamu ya Hizbullah ya Lebanon amesema kuwa, Marekani imetenda jinai nyingi dhidi ya wananchi wa mataifa mbalimbali ya dunia na kuiamini nchi hiyo ni ujuha na ujinga.
Sayyid HassanNasrullah amesema hayo jana kwa mnasaba wa Siku ya Vilema wa Vita ambayo huadhimishwa katika siku ya kumbukumbu ya kuzaliwa Abbas bin Ali bin Abi Talib, mashuhuri kwa lakabu ya Abul Fadhl na kueleza kwamba, Hizbullah inajifakharisha na vilema na majeruhi wake wa vita pamoja na subira kubwa waliyonayo.
Mbali na kuashiria kujitolea pakubwa wapiganaji wa muqawama na kueleza jinsi majeruhi wa vita walivyo na mchango mkubwa wa kutoa mwongozo kwa wananchi kutokana na subira na kusimama kwao kidete, Nasrullah amesema kuwa, vilema na majeruhi hao ni nyaraka na ushahidi wa wazi wa kuuendelezwa muqawama dhidi ya adui.

Katika sehemu nyingine ya hotuba yake, Katibu Mkuu wa Hizbullah ya Lebanon ameashiria matukio ya sasa ya Russia na Ukraine na kusema kuwa, mwakilishi wa Marekani anaihutubu Russia na kuiambia shambulio lolote lile dhidi ya raia ni jinai za kivita, lakini anasema nini kuhusu mauaji yaliyofanywa na Marekani katika vita vyake vyote?
Nasrullah amehoji kwa kusema, hivi Marekani ina cha kusema kuhusiana na mauaji yake katika maeneo mbalimbali ya dunia kuanzia Hiroshima na Nagasaki ambapo athari zake mbaya zipo mpaka leo, hadi huko Iraq na kuua makumi ya maelfu ya watoto wa nchi hiiyo, aua mauaji yake huko Afghanistan ambapo ndege za kivita za Marekani zimewashambulia kwa mabomu na kuwaua hata mabibi na mabwana harusi?