HAMAS: "Muqawama" ndiyo njia pakee ya kupambana na wavamizi na kuwashinda
Harakati ya Mapambano ya Kiislamu ya Palestina HAMAS imesema kuwa, njia pekee ya kuweza kupambana na kuwashinda wavamizi ni muqawama na mapambano ya kila upande, ya silaha, ya kisiasa, ya kijamii, ya kiuchumi na ya kidiplomasia.
HAMAS ilitoa tamko jana Jumatatu kuhusu kuongezeka vitendo vya kivamizi na jinai za utawala wa Kizayuni dhidi ya Wapalestina na matukufu yao na kusisitiza kuwa, muqawama ndiyo njia pekee ya ukombozi.
Katika kipindi cha wiki za hivi karibuni, wanajeshi makatili wa Israel wamezidisha jinai zao dhidi ya Wapalestina na kumeripotiwa kesi nyingi za kupigwa risasi za kivita Wapalestina tena moja kwa moja bila ya huruma na wanajeshi wa utawala wa Kizayuni.
Ripoti ya "Falastin al Yaum" imenukuu tamko la Harakati ya Mapambano ya Kiislamu ya Palesitna HAMAS likisema kwamba: "Muqawama ndiyo njia pekee inayoweza kuliongoza taifa la Palestina kwenye ukombozi wa ardhi zote zinazokaliwa kwa mabavu na Wazayuni."
Taarifa hiyo ya HAMAS imeongeza kuwa, muqawama hadi hivi sasa umepata mafanikio makubwa katika matukio na minasaba tofauti na kwa kweli hiyo ndiyo njia pekee ya ukombozi. Harakati hiyo aidha imewataka Wapalestina wote kuipa nguvu fikra ya ushirikiano wa kweli wa kitaifa na kufuata muongozo mkuu uliobuniwa na wanamapambano wa Kipalestina kwa ajili ya kuendeleza muqawama.
Kabla ya hapo pia, makundi ya muqawama ya Palestina yalikuwa yametoa onyo kali kwa utawala wa Kizayuni kwamba ndio utakaobeba dhima ya lolote litakalotokea kutokana na kuvamiwa Msikiti wa al Aqsa ambao ni Kibla cha Kwanza cha Waislamu na pia jinai zinazoendelea kufanywa na Wazayauni huko Baytul Muqaddas.