UN yataka kukomeshwa ubaguzi dhidi ya Waislamu wa Myanmar
Ripota Maalumu wa Umoja wa Mataifa katika Masuala ya Haki za Binadamu nchini Myanmar ametoa wito wa kukomeshwa ubaguzi dhidi ya Waislamu wa nchi hiyo.
Yanghee Lee amesema kuwa, serikali ya Myanmar inapaswa kukomesha mara moja ubaguzi unaofanywa dhidi ya Waislamu katika jimbo la Rakhine nchini humo.
Lee ameashiria safari yake ya hivi karibuni nchini Myanmar na kusema, ameshuhudia kesi nyingi za ubaguzi dhidi ya Waislamu katika jimbo la Rakhine na kwamba mwenendo huo unapaswa kukomeshwa.
Ripota Maalumu wa Umoja wa Mataifa Kuhusu Haki za Binadamu nchini Myanmar ameitaka serikali ya nchi hiyo kushughulikia hali ya wakimbizi Waislamu huko magharibi mwa nchi hiyo. Vilevile amekemea hatua ya serikali ya nchi hiyo ya kuhalalisha ukiukaji wa haki za binadamu za Waislamu kwa kutumia kisingizio cha kuimarisha amani na usalama.
Maelfu ya Waislamu wa jamii ya Rohingya wameuawa na wengine wengi kulazimika kuwa wakimbizi kutokana na mashambulizi ya kibaguzi yanayofanywa na Mabudha wenye misimamo mikali wakisaidiwa na jeshi la Myanmar.