Apr 24, 2024 12:24 UTC
  • Borrell: Uharibifu wa Israel huko Gaza unazidi uliofanywa katika miji ya Ujerumani katika Vita vya Pili vya Dunia

Mkuu wa Sera za Kigeni wa Umoja wa Ulaya amesema kuwa vita vya Israel dhidi ya Gaza vimesababisha uharibifu mkubwa kwenye miji ya eneo hilo kuliko ule uliosababishwa na Vita vya Pili vya Dunia kwenye miji ya Ujerumani.

Josep Borrell ambaye alikuwa akihutubia Bunge la Ulaya katika mji wa Strasbourg nchini Ufaransa amesema: "Tunaweza kusema kwamba zaidi ya 60% ya miundombinu ya Gaza imeharibiwa, na 35% imeangamizwa kikamilifu."

Borrell amedokeza kwamba wafanyakazi 249 wa masuala ya kibinadamu na waandishi wa habari wapatao 100 wameuawa katika mashambulizi ya Israel huko Gaza.

Amesema, "Israel inapaswa kuheshimu sheria za kimataifa, kutekeleza hatua za muda za Mahakama ya Kimataifa ya Haki, na kuhakikisha ulinzi wa raia wote."

Mkuu wa Sera za Kigeni wa Umoja wa Ulaya amekariri maonyo yake kwa Israel dhidi ya matokeo mabaya ya kulivamia eneo la Rafah kusini mwa Ukanda wa Gaza, ambapo Wapalestina wapatao milioni 1.4 wamekimbilia hifadhi, akisema kwamba hilo litasababisha maafa makubwa.

Ameongeza kuwa, "Ni muhimu Israel itekeleze azimio nambari 2728 la Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa, ambalo linasisitiza ulazima wa kufikishwa kikamilifu misaada ya kibinadamu huko Gaza."

Tangu mwezi Oktoba mwaka jana Israel imekuwa ikifanya mashambulizi ya kikatili dhidi ya watu wa Ukanda wa Gaza na hadi imeua zaidi ya Wapalestina elfu 34 wengi wao wakiwa wanawake na watoto wadogo.