Dennis Etler: Al-Qaida na ISIS yanatumikia maslahi ya Marekani
Mchambuzi wa masuala ya kisiasa wa nchini Marekani, amesema kuwa Washington haitaki kuyatokomeza makundi ya kigaidi ya Daesh (ISIS) na al-Qaida kwa kuwa, magenge hayo yanatumikia maslahi yanchi hiyo.
Dennis Etler, ambaye ni mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Aptus cha California nchini Marekani ameyasema hayo katika mahojiano aliyofanyiwa na kanali ya Press TV ambapo sambamba na kuashiria pendekezo la Wizara ya Ulinzi ya nchi hiyo Pentagon la kutaka kutuma askari zaidi nchini Afghanistan chini ya anuani ya kupambana na kundi la al-Qaida, amesema lengo la Washington la kutuma askari hao ni kusimamia mashamba yanayolima mpopi na biashara ya madawa ya kulevya aina ya heroini.
Amesema kuwa, hii ni kwa kuwa bidhaa hizo ndizo zinazoyadhaminia fedha makundi ya kigaidi ambayo yanapata uungaji mkono wa Marekani huko kaskazini mwa Afrika, Mashariki ya Kati na kusini mwa Asia, kwa sababu Shirika la Ujasusi la Marekani (CIA) linayadhaminia pesa makundi ya kigaidi nje ya mipaka ya Marekani kupitia fedha za magendo (Black Money.)
Akijibu swali kwamba ni kivipi Marekani inayaunga mkono makundi ya kigaidi katika hali ambayo imekuwa ikijinadi kwamba inaendesha vita dhidi ya magaidi? Dennis Etler amesema kuwa, Washington imeandaa mazingira ambayo magaidi sambamba na kuvuruga usalama wa maeneo muhimu ya kistratijia, yanaifungulia njia nchi hiyo kuweza kuingilia kijeshi katika maeneo hayo kwa kisingizio cha kupambana na makundi ambayo yenyewe ndiyo iliyoyaasisi.