Amnesty yaikosoa Israel kwa kuziuzia silaha nchi zinazokiuka haki za binadamu
https://parstoday.ir/sw/news/world-i53610-amnesty_yaikosoa_israel_kwa_kuziuzia_silaha_nchi_zinazokiuka_haki_za_binadamu
Shirika la kutetea Haki za Binadamu la Amnesty International limeukosoa vikali utawala wa Kizayuni wa Israel kwa kuendelea kuziuzia silaha na suhula za kiintelijensia nchi ambazo zinatambulikwa kwa ukiukakaji wa haki za binadamu.
(last modified 2023-11-27T12:14:11+00:00 )
May 20, 2019 11:03 UTC
  • Amnesty yaikosoa Israel kwa kuziuzia silaha nchi zinazokiuka haki za binadamu

Shirika la kutetea Haki za Binadamu la Amnesty International limeukosoa vikali utawala wa Kizayuni wa Israel kwa kuendelea kuziuzia silaha na suhula za kiintelijensia nchi ambazo zinatambulikwa kwa ukiukakaji wa haki za binadamu.

Katika taarifa, Amnesty imesema utawala wa Kizayuni unaendelea kuziuzia silaha nchi ambazo zimevunja rekodi ya kukiuka haki za binadamu kama vile Umoja wa Falme za Kiarabu, Sudan Kusini na Myanmar.

Tovuti ya habari ya Middle East Monitor imenukuu ripoti hiyo ya Amnesty International ambayo imekosoa vikali mwenendo huo wa Tel Aviv wa kuendelea kurundika silaha na vifaa vya kijasusi kwa nchi hizo zinazofahamika kwa kukanyaga waziwazi haki za binadamu.

Amnesty imeitaja hatua ya kampuni za silaha za utawala haramu wa Israel kama ukiukwaji wa sheria za kimataifa na sheria za ndani za utawala huo haramu.

Silaha za Israel zinavyotumika kuwaua Waislamu wa Rohingya

Imarati na Saudi Arabia zinaongoza muungano vamizi wa kijeshi ambao unaendelea kufanya mashambulizi dhidi ya wananchi wa Yemen tokea Machi mwaka 2015, ambapo makumi ya maelfu wameuawa na kujeruhiwa, mbali na mamilioni kulazimika kuwa wakimbizi.

Hali kadhalika Kamisheni Kuu ya Haki za Binadamu ya Umoja wa Mataifa mara kwa mara imekuwa ikitoa mwito wa kutouziwa silaha jeshi la Myanmar ambalo linafanya ukatili wa kutisha dhidi ya Waislamu wa jamii ya Rohingya, kwa kushirikiana na Mabudha wenye misimamo ya kuchupa mipaka.