Kisingizio cha Marekani cha kutaka kuwepo kijeshi Sudan Kusini
Marekani imedai kuwa kuwepo wanajeshi wake huko Sudan Kusini kutasaidia kuhitimisha machafuko ya kisaisa na mashambulizi ya wabeba silaha nchini humo.
John Kerry Waziri wa Mashauri ya Kigeni wa Marekani amedai leo Alhamisi baada ya kukamilisha ziara ya siku mbili huko Kenya na Nigeria kuwa kuwepo wanajeshi wa Marekani huko Sudan Kusini kunaweza kusaidia kurejeshwa amani nchini humo; huku weledi wa mambo wa kieneo wakiamini kuwa kuweko vikosi vya Marekani barani Afrika siku zote kumekuwa kukiambatana na wimbi la machafuko na ukosefu wa amani.
Madai hayo ya John Kerry yamekosolewa na taasisi za kiraia na kijamii kufuatia kuongezeka wimbi la mashambulizi ya makundi yenye silaha huko Sudan Kusini ambapo hadi sasa watu 300 wameuawa na kuisababishia nchi hiyo matatizo mbalimbali ya kiuchumi. Mmoja wa wasemaji wa jeshi la Marekani ametangaza kuwa Washington imetuma wanajeshi 40 katika mji mkuu wa Sudan Kusini, Juba ili kuwalinda wafanyakazi wa ubalozi wake, kufuatia kushtadi machafuko katika nchi hiyo ya Kiafrika.
Katika ziara yake nchini Kenya, Kerry alishiriki kwenye kikao cha kieneo chini ya anwani "Usalama na Mapambano dhidi ya Vita vya Ndani" kilichohudhuriwa na Mawaziri wa Mambo ya Nje wa Kenya, Uganda, Sudan Kusini, Djibout, Tanzania, Somalia na Ethiopia huko Nairobi.