Polisi Kongo yawatia mbaroni makumi ya raia
Polisi wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo wamewatia mbaroni makundi ya raia kwa kosa la kushiriki maandamano dhidi ya serikali.
Polisi wa Kongo jana walipambana vikali na raia waliokuwa wakiandamana katika mitaa mbalimbali ya mji mkuu Kinshasa kupinga siasa za Rais Joseph Kabila wa nchi hiyo, maandamano ambayo yalisababisha kutiwa nguvuni watu 275.
Habari zinasema kuwa ghasia zinaendelea katika miji mbalimbali ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo huku askari polisi wakitumia gesi iya kutoa macho kuwatawanya raia.
Ida Sawyer, Mkurugenzi wa eneo la Afrika ya Kati wa Human Rights Watch amesema, watu 19 wameuliwa na maafisa usalama katika maandamano mjini Kinshasa, watano mjini Lubumbashi na sita katika miji ya bandari ya Goma na Matadi, magharibi mwa nchi hiyo.
Hata hivyo serikali ya Kinshasa imesema ni watu 22 pekee waliouawa katika makabaliano kati ya waandamanaji na maafisa usalama na kwamba polisi kadhaa pia wameuawa. Viongozi wa Kongo wamepiga marufuku maandamano ya wapinzani.
Inafaa kuashiria hapa kuwa, kwa mujibu wa katiba ya Kongo, Rais Joseph Kabila hastahiki kugombea kiti cha rais kwa mara nyingine baada ya kumalizika muhula wake wa uongozi mwezi huu wa Disemba.