Wafuasi 20 wa Mursi wahukumiwa adhabu ya kifo Misri
Mahakama Kuu ya Misri imewahukumu wafuasi 20 wa rais aliyeondolewa madarakani wa nchi hiyo adhabu ya kifo kwa madai kwamba wamepatikana na hatia ya kuua polisi 13.
Miaka minne baada ya ghasia na machafuko makubwa yaliyosababishwa na kuondolewa madarakani Muhammad Mursi, rais wa kwanza kuchaguliwa kwa njia za kidemokrasia nchini Misri, Mahakama Kuu ya nchi hiyo jana ilitoa hukumu ya kifo dhidi ya wafuasi wake 20 kati ya 149 waliofikishwa mahakamani hapo.
Mwezi Agosti mwaka 2013 wafuasi waliokuwa na hasira wa Muhammad Mursi walishambulia kituo cha polisi katika viunga vya mji wa Cairo na kuua polisi 13 baada ya jeshi la polisi kushambulia maandamano yao na kuua zaidi ya raia mia saba.
Baada ya jeshi la Misri kumuondoa madarakani Muhammad Mursi kutoka harakati ya Ikhwanul Muslimin hapo mwaka 2013, serikali ya Cairo ilipiga marufuku shughuli zote za harakati hiyo. Vilevile idadi kubwa ya viongozi na wanachama wa harakati hiyo wamefungwa jela na baadhi yao wamehukumiwa adhabu ya kifo.