Wasiwasi wa kuongezeka idadi ya wakimbizi DRC, wazidi kuwa mkubwa
Umoja wa Mataifa umetangaza kuwa, makumi ya maelfu ya watu wamekimbia makazi yao katikati mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo na kukimbilia kusini mwa nchi hiyo.
Ofisi ya Uratibu wa Masuala ya Kibinadamu ya Umoja wa Mataifa huko Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo imesema kuwa, karibu wakimbizi 45 elfu wamekimbia makazi yao kutokana na kushadidi mapigano baina ya makundi yenye silaha katika jimbo la Kasai la katikati mwa nchi hiyo, na wameelekea upande wa kusini mwa nchi hiyo kubwa ya katikati mwa Afrika.
Kwa mujibu wa ripoti hiyo, majina ya wakimbizi hao na idadi yao imeorodheshwa katika jimbo la Lualaba la kusini mwa nchi hiyo.
Kabla ya hapo Umoja wa Mataifa ulikuwa umetangaza kuwa, mapigano kati ya makundi ya wanamgambo yamepelekea maelfu ya wakazi wa katikati mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo kukimbilia maeneo mengine ya nchi hiyo na pia katika nchi jirani ya Uganda tangu mwezi Machi mwaka huu.
Kupigania udhibiti wa maeneo pamoja na utajiri wa maliasili za maeneo hayo ni miongoni mwa sababu kuu za kutokea mapigano ya mara kwa mara baina ya makundi ya waasi huko Jamhuri ya Kidemorasia ya Kongo.