FAO yachukua hatua kuzuia makali ya kiangazi Somalia
https://parstoday.ir/sw/news/africa-i29968-fao_yachukua_hatua_kuzuia_makali_ya_kiangazi_somalia
Shirika la Chakula na Kilimo la Umoja wa Mataifa (FAO) limetibu mifugo zaidi ya milioni 12 chini ya miezi mitatu iliyopita, kwa shabaha ya kudhibiti makali ya ukame na baa la njaa nchini Somalia.
(last modified 2023-11-27T12:14:11+00:00 )
Jun 03, 2017 07:17 UTC
  • FAO yachukua hatua kuzuia makali ya kiangazi Somalia

Shirika la Chakula na Kilimo la Umoja wa Mataifa (FAO) limetibu mifugo zaidi ya milioni 12 chini ya miezi mitatu iliyopita, kwa shabaha ya kudhibiti makali ya ukame na baa la njaa nchini Somalia.

Shirika la habari la Tasnim limemnukuu Richard Trenchard, Mjumbe wa FAO nchini Somalia akisema kuwa, shirika hilo la UN linatazamia kutibu mifugo milioni 22 kufikia katikati ya mwezi huu wa Julai, ambayo ni chanzo cha riziki kwa Wasomali milioni 3.

Kwa mujibu wa FAO, watu milioni 3.2 wa Somalia wapo katika hatari ya kupoteza maisha kutoka na baa la njaa.

Nembo ya Shirika la Chakula na Kilimo la Umoja wa Mataifa 

Shirika la Chakula na Kilimo la Umoja wa Mataifa (FAO) limetuma madaktari 150 wa mifugo kutibu mbuzi, kondoo, ng'ombe na ngamia karibu 270,000 kila siku katika nchi hiyo ya Pembe ya Afrika.

Mwezi Machi mwaka huu Kostas Stamoulis, Naibu Mkurugenzi Mkuu Shirika la Chakula na Kilimo la Umoja wa Mataifa (FAO) alitahadharisha kuwa, ukame na vita vitaifanya hali ya chakula kuwa mbaya sana barani Afrika hususan katika baadhi ya maeneo ya mashariki mwa bara hilo.