Bunge la Zambia lawatimua wabunge waliosusia hotuba ya rais
Bunge la Zambia limewafukuza makumi ya wabunge wa upinzani ambao walisusia hotuba ya Rais Edgar Lungu wa nchi hiyo miezi michache iliyopita.
Patrick Matibini, Spika wa Bunge hilo amesema kuwa: "Natumia mamlaka yangu ya kisheria kuwafukuza wabunge 48 wa chama cha upinzani cha United Party for National Development (UPND), kwa kipindi cha siku 30, kwa kuondoka nje ya Bunge mwezi Machi, wakati wa hotuba ya Rais Lungu."
Amesema iwapo wabunge hao hawamtambui rais aliyechaguliwa na wananchi kwa njia halali, basi wana khiari ya kujiuzulu. Wabunge hao wa upinzani walitoka nje wakisema kuwa hawamtambui Rais Lungu kuwa ndiye mshindi halali wa uchaguzi wa Agosti mwaka jana.
Spika wa Bunge la Zambia amesema wabunge hao wa chama cha UPND hawatolipwa mshahara katika muda huo wa mwezi mmoja wala kuruhusiwa kukaribia maeneo ya bunge.
Hii ni katika hali ambayo, Hakainde Hichilema, kiongozi wa upinzani aliyewania kiti cha urais katika uchaguzi uliopita na kutoa upinzani mkali kwa Rais Edgar Lungu ameshtakiwa kwa makosa ya uhaini na yupo kizuizini tangu Aprili.
Katika uchaguzi huo wa Agosti 11 mwaka jana, licha ya matokeo ya awali ya uchaguzi huo kuonyesha kuwa, Hakainde Hichilema anaongoza, lakini matokeo yaliyokuja kutangazwa baadaye na Tume ya Uchaguzi yalionyesha kuwa, Rais Edgar Lungu ndiye aliyekuwa mshindi wa kiti cha urais baada ya kujikusanyia asilimia 50 ya kura jambo ambalo liliibua mgogoro mkubwa wa kisiasa unaoendelea kutokota nchini humo.